1.Jifunze kuzuia ulimi wako usinene mabaya – Mtume Petro anatueleza kwamba ‘Kwa maana, Atakaye kupenda maisha, Na kuona siku njema, Auzuie ulimi wake usinene mabaya, Na midomo yake isiseme hila’ (1Petro 3:10). Ikiwa unataka kuwa na maisha yenye furaha na amani (siku njema) basi chunga sana unayoyasema. Ukiruhusu kinywa chako kunena mabaya na kutunga hila usitegemee kuwa na amani ya kweli, maana utaishi kwa maneno hayo. Daima usiakiache kinywa chako kinene mabaya wala kutunga hila kwa kuwa mtu azuiaye kinywa chake kunena mabaya, huilinda nafsi yake na taabu (Rejea Mithali 21:23 & Zaburi 50:19). Kumbuka unaponena mabaya juu ya mwingine, kama mtu huyo hana Yesu aliye hai wa kumuongoza kusamehe, basi ujue ndani yake unaamsha roho ya kisasi na uharibifu. Wapo pepo ambao kazi yao ni kufuatilia nini mtu anajinenea au kunena juu ya mwingine hususani yale ambayo ni mabaya, na kazi yao kufuatilia maneno hayo kuhakikisha kwamba yanatimia au yanatokea.
Jizuie kunena unapokuwa na hasira – Katika Waefeso 4: 26 imeandikwa
‘Mwe na hasira, ila msitende dhambi; jua lisichwe na uchungu wenu bado haujawatoka’ . Mara nyingi kwenye jambo hili watu wengi wameshindwa kujizuia, na ukitaka ujue yaujazayo moyo wa mtu au mtu anakuwazia nini subiri azungumze habari zako au mambo yako akiwa amekasirika. Hasira ni mlango ambao adui anautumia sana kuharibu maisha ya watu wengi na hasa wanandoa kwa sababu ya yale ambayo kila mmoja aliyanena akiwa na hasira na uchungu juu ya mwenzake. Biblia inatuambia kunyamaza ni hekima, hivyo jifunze kunyamaza. ‘Hata mpumbavu akinyamaza, huhesabiwa hekima; Akifumba midomo yake, huhesabiwa ufahamu’ (Mithali 17:28).
Jifunze kulinda kinywa chako – ukienda kwenye Mithali 13:3 Biblia inasema ‘Yeye alindaye kinywa chake hulinda nafsi yake, bali afunuaye midomo yake atapata uharibifu’ . Naam watu wengi hawajui kwamba kadri unavyosema maneno mabaya, ya uongo, kusengenya au kusingiza au kuchafua nk, ndivyo wanavyojitengenezea mazingira ya uharibifu kwenye maisha yao binafsi na si tu kwa wale ambao wanawaelekezea maneno husika.Katika Mithali 21:23 imeandikwa ‘Mtu azuiaye kinywa chake na ulimi wake, Atajilinda nafsi yake na taabu’. Hii ni kwa sababu maneno unayoyanena unayaumba au kuyaandika na kwa jinsi hiyo maneno hayo yana nguvu ya kuongoza na kuathiri hisia, nia na maamuzi (matendo) yako.
Jifunze kuwa mtu wa maneno machache – Biblia inatuambia ‘Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili’ (Mithali 10:19). Naam sio lazima kusema kila neno linalokujia jifunze kunyamaza na kuzuia maneno yako, maana azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa. Ingawa Yakobo anatuambia ulimi haufugiki, lakini kwa mujibu wa (Mithali 17:27a) mtu anaweza kuzuia maneno yake na hiki ndicho alichomaanisha Mzee Yakobo mwenyewe pale aliposema iweni wepesi wa kusikia na si wepesi wa kusema (Yakobo 1:19).
Jifunze kufikiri kabla hujanena – Katika Mithali 12:18 imeandikwa
‘Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; Bali ulimi wa mwenye haki ni afya. Naamini umeshawahi kupitia mazingira ambayo unajutia maneno uliyoyanena. Mara nyingi majuto hayo ni matokeo ya kunena bila kufikiri. Hii ina maana kabla ya kusema, jifunze kufikiri kwanza athari ya unachotaka kusema kwa mtu au watu unaotaka kusema nao. Katika kufanikisha hili mwimbaji wa Zaburi akasema ‘Ee Bwana, uweke mlinzi kinywani pangu, Mngojezi mlangoni pa midomo yangu’ (Zaburi 141:3).
Jaza neno la Mungu moyoni mwako
(Yoshua 1:8) – Hii ni kwa sababu yale yaujazayo moyo wa mtu ndiyo yamtokayo. Hivyo ili kusaidia kinywa chako kutoa maneno yenye kujenga sharti neno la Mungu likae kwa wingi moyoni. Hatutegemei mtu aliyejaa neno la Mungu atukane watu, kulaani, kusengenya nk. Katika Yakobo 3:9-10 imeandikwa ‘ Kwa huo twamhimidi Mungu Baba yetu, na kwa huo twawalaani wanadamu waliofanywa kwa mfano wa Mungu. Katika kinywa kile kile hutoka baraka na laana. Ndugu zangu, haifai mambo hayo kuwa hivyo’ . Naam ile kusema haifai mambo hayo kuwa hivyo ni ishara kwamba hatupaswi kutumia vinywa vyetu kunena mabaya na kutunga hila wakati tunatumia pia ulimi huo huo kumtukuza Mungu.
Katika kumalizia ujumbe huu sina budi kusema mwanadamu hana budi kuwa makini sana na kinywa chake. Maisha ya mtu yanachangiwa kwa sehemu kubwa na maneno yake, akiutumia vizuri ulimi wake ataishi vizuri na akiutumia vibaya mabaya yatakuwa haki yake. Naamini ujumbe huu mfupi umekuongezea ufahamu wa kutosha mosi kuhusu Biblia inasema nini juu ya ulimi na pili namna ya kukitumia kinywa chako vizuri ili kuamua hatma nzuri ya maisha yako.
‘Na ulimi wangu utanena haki yako, Na sifa zako mchana kutwa’ (Zaburi 35:28)
Utukufu na Heshima vina wewe Yesu wangu, wastahili BWANA.
Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, iwe nanyi.
No comments:
Post a Comment